UWIANO WA MALI (ASSETS) NA MADENI (LIABILITIES) KATIKA BIASHARA
Watu wengi wanapopata pesa nyingi kwa mkupuo (mara moja) mfano mshahara, pensheni, dili n.k hukimbilia kununua vitu kama mashamba, fenicha za ndani (kitanda, makochi), wakidhani kuwa hapo wamenunua assets. Too bad ni kwamba watu hujiingiza katika hali ya madeni (liabilities) ambayo huwadhoofu sana kiuchumi. Sasa leo tuone uwiano wa Mali (assets) na madeni (liabilities) katika biashara, ukweli ni upi? wapi ukuwekee umakini? Makinika…
Kwanza jiulize, tunaposema hii ni Mali (Asset) maana yake nini? Na tunaposema hili ni deni (liability) maana yake nini. Saa zingine mambo hayako vile ambavyo unaweza kutafsiri kirahisi.
ASSET: Hii ni ile mali ambayo unitumia kuingiza pesa katika biashara yako. Ngoja nikuulize, katika mali zako zote ambazo unazo, ngapi zinakuingizia pesa kila siku/kila baada ya muda fulani? Jibu unalo mwenyewe. Kama una mali (simu, nyumba, gari, laptop, friji n.k) na bado mali hio haikuingizii Pesa, hapo huna Asset bado ndugu.
LIABILITY: Hii ni ile kitu ambayo haikuingizii pesa na badala yake, Kitu hii inafyonza pesa katika mifuko yako. Mfano mzuri ni Simu za vijana wengi, yani unakuta kijana anatumia simu ya gharama, kaiwekea cover la gharama, protector ya kijanja na Bando haliishi. Lakini kijana huyo hajawahi kiutumia simu yake hio anayotamba nayo kuingiza pesa. Kama unahisi nakufokea hapa nisamehe tu. Lakini kufikia hapo simu hio inageuka Deni/Mzigo/Liability. Kwasababu haikusaidii kuingiza pesa, hio ni liability tu. Mfano mwingine wa liability ni nyumba ya kuishi, gari ya kutembelea, mkopo, Kuwa na wanawake wengi (kama wewe ni mwanaume), starehe na maisha ya anasa.
Watu wengi hasa vijana hujikuta wana Liabilities nyingi kuliko Assets, lakini ukimuuliza anakwambia ana assets nyingi kwa kuwa amenunua vitu vingi geto na anatembelea gari nzuri mjini, utamwambia nini apo?
KIBIASHARA IMEKAEJE HII?
Biashara ili iwe imara, inapaswa kuanza kidogo na kisha kukua taratibu bila kuruka stage. Yani kama mtoto mdogo tu, lazima anyonye, atambae, ajifunze kuongea, atembee na kuanguka mara kadhaa kabla hajaanza kukimbia, kutumwa dukani na kuanzishwa shule. Kama ni hivyo kwanini ewe mjasiriamali uliyeanza biashara huna hata miaka miwili ukate tamaa? Hakuna kuruka stage hapa. Na ili uweze kwenda sawa sawa unapaswa kukusanya Assets nilizoelezea leo hapo juu achana na achana na zile ulizokariri shuleni kwenye book-keeping hapo kabla.
Mfano wa assets katika biashara ni Website nzuri iliyounganishwa na teknolojia ya S.E.O, akaunti hai za mitandao ya kijamii kama facebook, instagram, youtube, twitter nk, laptop, simu, printer, jengo la ofisi, connections zako na watu mbalimbali mjini (yes connection ni asset.) pamoja na vifaa vingine unavyovitumia kila siku katika biashara yako. Vipi hapo umeshaanza kupata picha kuhusu uwiano wa Mali (assets) na madeni (liabilities) katika biashara? Tuendelee..
Kufahamu vizuri kuhusu namna ya kutumia teknolojia ya S.E.O kwa manufaa katika biashara yako fuatana na makala hii hapa..
NINAWEZA VIPI KUBADILI MADENI (LIABILITIES) ZANGU KUWA MALI (ASSETS)?
Hili ni swala la ukomavu na maamuzi magumu. Liabilities zako kama smartphone, laptop, gari nakadhalika, unaweza kuzibadili kutoka kuchati, kuangalia muvi na kupigia misele kwa pisi kali mpaka kuweza kukuingizia pesa nzuri.
Mohammed Dewji (@moodewji ) aliwahi kutweet kutushauri vijana kuhusu “Kuongeza Mali na kupunguza Madeni” na bahati nzuri kuna mdau mmoja alinijia nimuelezee, pale Bro alimaanisha nini il’hali pesa ya kujikimu tu bado haitoshi? Nakwambia, hii ndio maana ya ile tweet ya bro Mo Dewji, kwamba hakikisha Assets zinaongezeka kwa kasi zaidi kuliko kasi ya kuongezeka kwa Liabilities. Hapa kuna mtihani mkubwa sikufichi. Maisha ya Watu wengi huongezeka gharama pale kipato kinapozidi kuwa kikubwa.
Angalia mfano huu kutoka katika kitabu maarufu cha “Rich Dad Poor Dad“

Ndipo utaelewa kwa nini masikini wanazidi kuwa masikini, Watu wa uchumi wa Kati (mnajijua) wanazidi kukimbizana na mbio za panya, na matajiri wanazidi kuwa matajiri. Narudia ili uweze kubadili Liabilities zako ziwe Assets unahitaji kuwa Mkomavu na Kuchukua Maamuzi Magumu.
Hayo maamuzi magumu yanapaswa kuongozwa na ile Kiu ya kutaka kufanikiwa, sio uchawi na mambo ya kurudishana nyuma. Na pia kuwa Mkomavu unapaswa kuwa misuli katika akili yako. Kama ilivyo misuli ya mwili inahitaji mazoezi ili iweze kuwa Imara na yenye nguvu, kadhalika misuli ya akili yako. Hapa ili akili yako iwe na misuli imara kwanza jiweke kwenye MAZINGIRA ya watu wenye akili na waliofanikiwa kukuzidi. Watoto wa mjini wanaita Koneksheni. Hii ndio asset namba moja.
Ukiweza kubadili na kuimarisha mazingira yanayokuzunguka kwanzia kwa watu wako unaowashirikisha shughuli zako za kila siku, Akili inaanza kukomaa, na automatically unakuwa unao uwezo wa kufanya maamuzi magumu kuhusu hali yako ya Uchumi na Biashara yako. Ukiwa na akili Hasi hapa hutaweza kunielewa kamwe. Hebu fungua hicho kichwa vizuri kabisa kwanza.
IFAHAMU BALANCE SHEET KATIKA KUUTAFUTA UWIANO WA MALI (ASSETS) NA MADENI (LIABILITIES) KATIKA BIASHARA
Licha ya kuwa ni kitabu cha kihasibu, lakini ni muhimu sana katika utendaji wa biashara yoyote na/uchumi binafsi wa mtu yeyote. Kitabu hiki ndicho kinachoweza kukuonyesha afya ya biashara yako au uchumi binafsi. Tizama mfano huu kisha ili uweze kutengeneza Balance Sheet yako binafsi chora alama mfano wa “T” katika karatasi kisha Upande mmoja uite ASSETS kisha orodhesha mali zako zote ambazo zinakuingizia pesa kila siku. Upande wa pili uite LIABILITIES kisha orodhesha mali zote mabazo zinakugharimu pesa bila kuingiza ili kuziendesha.
Ukishafanya hivyo, utakachokipata ndicho kitakupa hali yako kiuchumi ya sasa (kama ni Masikini, mtu wa Uchumi wa kati au Tajiri). Kwa manufaa zaidi zoezi hili unaweza kulifanya kila Unapoanza mwaka mpya. Ule muda watu wamekomaa kuandika Resolutions zao wewe tengeneza Balance sheet yako, kisha ifanyie kazi kwa kuongeza orodha ya Assets na kujitahidi kupunguza/kutoongeza Liabilities zisizo na maana. Kwa hakika kila mwaka mpya ukifanya hivi, matokeo chanya lazima uyaone.
UTAJIRI (NET WORTH) UNAPIMWA VIPI?
Najua umeshawahi mara nyingi tu kuona ile orodha watu matajiri zaidi duniani. Unajua wanapimaje utajiri huo il’hali hawajui hata masalio ya watu hao katika benki wanazohifadhi pesa zao. Leo nakujuza sasa. Hesabu ni ile ile: Orodhesha Assets zote alizonazo mtu fulani unayemfahamu, kumbuka hapa assets tunazoziongelea ni zile mali zinazoingiza pesa tu. Kisha tafuta thamani yake. Halafu orodhesha Liabilities zake zote unazozifahamu (zile mali zinazomfyonza pesa). Ukimaliza fanya hivi; ASSETS – LIABILITIES = NET WORTH

Hesabu hii ukitaka iseme ukweli kabisa anza kujipigia wewe mwenyewe, uone jinsi gani unapoteza muda hapa duniani kupiga umbea na kufanya mambo yasiyo na maana. Unavyochora ile Balance sheet yako pale kila mwanzo wa mwaka, piga na hii Net Worth yako, ili ujue kabisa huo mwaka unaoanza unapaswa kuwa serious namna gani. Kifupi hizo ndizo Assets na Liabilities katika uchumi binafsi na uchumi wa kibiashara. Kwa maana ili biashsra iweze kumea vyema basi Mtendaji hana budi kuwa muumini namba moja ws falsafa bora za kibiashara, na falsafa bora ndizo hizi.
Ni matumaini yangu makala hii ya leo kuhusu uwiano wa Mali (assets) na madeni (liabilities) katika biashara, ukweli ni upi? basi umepata majibu ya maswali yaliyokuwa yanakusumbua. Una lolote la kuchangia? Tafadhali comment hapo chini na endelea kufuatilia makala zetu nyingine nyingi kupitia tovuti yetu maridhawa ya Rednet Technologies ili usipitwe daima.
Twende pamoja kidijitali kupitia makala zifuatazo ili upate muendelezo mzuri wa mada hii ya leo. Gusa link kisha makinika.
- UKIRITIMBA KATIKA BIASHARA, NI ASALI AU SHUBIRI?
- IJUE NGUVU YA MITANDAO YA KIJAMII KATIKA BIASHARA YAKO
- FAHAMU SIRI YA KUFANIKIWA KATIKA KUWEKEZA
Je umependezwa na makala yetu hii ya leo?
Unataka kufanya malipo kwa huduma zetu bila kuhofia makato ya miamala?
Sasa tumekuletea huduma ya LIPA NAMBA ya M-PESA (TILL NUMBER) – 5432715 ambapo unaweza kututumia TIP ya kutupongeza kwa kazi nzuri au Kulipia huduma unazozipata kutoka kwetu BILA MAKATO ya miamala.
Tumia LIPA NAMBA yetu muda wowote yaani 24/7.
